Search
Free School Management System
Free School Management System for Kenya

Free School Management System

Learn More

2015 KCSE Kajiado County Joint Examination

Kiswahili Paper 2

1. UFAHAMU (Alama 15)

Soma taarifa ifuatayo kisha ujibu maswali yanayofuatia
1.

Taifa, liwalo lolote, hupenda kuona maandishi yake yako kwenye kiwango cha juu Maandishi ni sehemu ya utamaduni na hakuna taifa linalopenda kuona utamaduni wake uko chini au unadhauliwa na mataifa mengine, Kadiri taifa linavyostawi ndivyo linavyopenda kuwa na maandishi yenye kiwango cha juu, kwani hili huleta fahari:”Maandishi haya yameandikiwa na watu wanaowaza,” kila taifa hupenda kusikia mataifa mengine yakisema hivyo kuhusu maandishi yake. Mhakiki ana dhima ya kusema wazi kuhusu kiwango cha maandishi huyu asilia atakapoamua kutunga tena, atashawishika kuandika maandishi yaliyo kwenye kiwango cha juu zaidi. Na waandishi wengine watapatiwa msukumo wa kuandika maandishi yaliyo kwenye kiwango cha juu pia na hivi ndivyo mhakiki anavyosaidia kukuza na kuendeleza maandishi ya taifa lake.

Mhakiki hujiuliza ni kiwango gani mwandishi amefaulu kuwachora wananchi katika harakati zao na kwa kiwango gani ameandika au ameyajadili matatizo yanayoisakama jumuiya hiyo? Je, ni kwa kiwango gani maandishi hayo yatawafanya wauelewe zaidi unyonge wao na kupambana na sababu za unyonge huo? Je,mwandishi amefaulu kwa kiwango gani kupambanua baina ya maadui wa jumuiya hiyo? Ni kwa kiwango gani amepambanua baina ya amali zinazoisaidia jamii kusonga mbele na zile zinazoizorotesha jamii hiyo? Swali hili ni swali la mtazamo.

Mhakiki lazima awe akili pevu sana ili aweze kung’amua mambo na akisha yang’amua ayaandike kwa lugha nyepesi, ili mawazo yake yasomeke na kila mtu kwa urahisi. Lugha ngumu na rahisi ni zipi? Hili ni tatizo ambalo mhakiki anapaswa kulielewa na kulitatua; anapaswa kushirikiana na watu wa kila namna ili aelewe wanaongeaje, na atumie lugha yao inapowezekana na inapofaa, kwa kifupi, atumie lugha ambayo itawatumikia wasomi wake.

Ni kiwango gani maandishi hayo yanawazindua na kuwapevusha wasomaji, ni jambo jingine ambalo mhakiki hujishughulisha nalo kila anapofanya uhakiki. Yawapevushe kimawazo na kimtazamo kwa jumla na yajaribu kuwafundisha namna ya kuepukana na kupambana na matatizo yao, yawapevushe ili waweze daima kutambua mawazo au watu gani wanaweza kuwa hatari na sumu kwao. Mhakiki huwasaidia wasomaji kuyabaini maandishi yaliyo sumu kwa jamii na atawasaidia hasa iwapo yeye mwenyewe ni sehemu ya wale wanaopambana na kupigania haki zao. Kuna maandishi mengine ambayo ni mazuri sana na yanagusa hisia za wasomaji kikweli sababu yameandikwa na watu wenye uwezo na fani kupindukia Maandishi hayo ni kama sambusa ambayo juu inametameta lakini ndani imeshindiliwa pilipili nyingi mno. Mhakiki sharti aseme wazi- ayafichue maandishi ya namna hiyo. Kuna maandishi ambayo huwachekesha na kuwaburudisha wasomaji, sababu yameandikwa kwa
namna hiyo; na kumbe yanaeneza sumu, na maandishi mengine ingawaje si sumu, huwa pale ili kufurahisha na kuchekesha tu. Kicheko kinasaidia nini? Maandishi haya yanazorotesha harakati kwa kuwachelewesha watu kusoma maandishi yao wote. Mhakiki ni lazima ajiendeleze katika taaluma mbalimbali ili aweze kuwa na mawazo mengi ambayo yatamsaidia kuhakiki maandishi mbalimbali. Mhakiki hodari huichonga jamii yake kimawazo, huimarisha isitetwereshwe na kupofushwa wapotoshi.

Baadhi ya waandishi asilia hueneza kasumba, pengine hufanya vile bila kujitambua Mhakiki lazima awafichue waandishi wanaoeneza mawazo ya kikasumba yasije yakaiambukiza jamii. Mhakiki ni lazima ayafichue na kuyaweka hadharani mawazo yote ya hatari yanayoenezwa kwa makusudi au kwa kutojua kwa waandishi asilia, kuna baadhi ya watu ambao hupenda kuhakiki vitabu vya watu wanaowaheshimu au marafiki zao, ili kuufanya urafiki baina yao ukomae zaidi, na mara nyingi hujikuta wanaandika muhtasari tu wa maandishi hayo na kujaza sifa kemkem: kamwe siwaiti wahikiki- hawa ni watu hatari sana kwa sababu hawamsaidii mwandishi asilia kujisahihisha ila(kwa kutojua au kwa makusudi) hujiunga na mwandishi asilia, kuizamisha jamii nzima. Lipo kundi jingine ambalo nalo siliiti la wahakiki kundi hili huangalia Fulani ametunga nini na kuanza kuponda vitabu vyake sababu wana fitina zao za siri. Makundi yote haya ni ya hatari sana katika taifa zima, mhakiki asiwe mlevi wa aina yoyote-asilewe Chuki au mapenzi kuhusu watu ambao maandishi yao anayahakiki. Lazima awe razini, asiwe hayawani. Ama sivyo, atakuwa mbomoaji, dufu la mtu.

Maswali ya ufahamu
a) Ipe taarifa hii anwani mwafaka. (alama 1)
b) Mhakiki ana jukumu gani kwa (alama 2)
i. Mwandishi
ii. Msomaji
c) Maandishi huwezaji kugusa hisia za wasomaji? (alama 2)
d) Fafanua ni vipi maandishi huwazindua na kuwapevusha wasomaji. (alama 2)
e) Bainisha aina tatu za wahakiki. (alama 3)
f) Kwa nini mwandishi wa taarifa hii haoni faida ya maandishi yanayochekesha? (alama 2)
g) Eleza maana ya kifungu kifuatacho cha maneno kama kilivyotumika katika taarifa. (alama 1)
Dufu la mtu

15 marks

2.UFUPISHO (Alama 15)

Soma habari ifuatayo kisha ujibu swali
2.

Mwana wa Adamu ni kiumbe cha ajabu! Ni kiumbe kilichopewa uwezo wa kuhodhi na kumiliki kila kitu, kiumbe kilichopewa akili na maarifa fuvu tele ili kutaratibu shughuli na mambi: kiumbe kilichopewa uwezo wa kuwasiliana na kutumia sauti nasibu ili kuwa na urari na muwala; kiumbe kilichopewa uwezo wa kufaidi viumbe wengine kwa njia mbalimbali na jumla jamala; hiki ndicho kiumbe kilichopewa idhini maalum ya kuzaana na kujaza dunia. Huyu ndiye mwana wa mama Hawa ambaye sasa amegeuka ndovu kumla mwanawe.

Kwa sababu ya bongo alizonazo, binadamu ana uwezo wa kutumia teknolojia kwa manufaa yake na ithibati zipo tele. Binadamu ametumia nyambizi kuzuru chini ya bahari, amefika mwezini, amevumbua magala: amevumbua uyoka: amevumbua tarakilishi na sasa shughuli zake ni za kutandaridhi. Mwenyewe yuasema kuwa dunia yake imekuwa kitongoji katika muumano huu.

Chambilecho wavyele, akili nyingi huondoa maarifa. Binadamu amekuwa dubwana linalojenga kushoto na kubomoa kulia na tuna sababu ya kulisoza dubwana hili kidole. Rabana ndiye msanii asiye mfanowe kwani aliisawiri murua. Rabuka akaona yote yalikuwa mema na mazuri: akamwambia binadamu,” Haya twende kazi!”

Viwanda vya binadamu vinatiririsha maji-taka ovyo hadi mitoni, maziwani na baharini na matokeo yamekuwa ni vifo vya viumbe vya majini kama samaki ambavyo ni urithi aliopewa na muumba. Hakuna kiumbe kinachoweza kustahimili maisha bila maji safi. Maji yote sasa yametiwa sumu na binadamu kwa sababu ya ‘maendeleo’ yake.

Joshi kutoa katika viwanda vivyo hivyo nalo limehasiri ukanda wa ozone ambao sasa umeruhusu jua kutuhasiri kwa joto kali mno. Siku hizi inasemekana kuwa kuna mvua ya aside inayonyesha katika baadhi ya sehemu za dunia na kuleta madhara makubwa. Labda hata mabahari yamekasirika kwa sababu hivi majuzi katika kile kilichoitwa ‘tsunami’, bahari lilihamia nchi kavu na kusomba maelfu ya binadamu na kuwameza wazima wazima.

Vimbunga navyo vimetokea kwa wingi. Wataalamu wanasema kuwa viwango vya miyeyuko vitazidi kwa sababu ya joto na kiwango cha maji kitazidi pia. Binadamu atatorekea wapi?
Idadi ya binadamu imezidi hadi kiasi asichoweza kukishughulikia kwa sababu anaijaza kiholela kwa sababu anadai kuwa aliruhusiwa kuijaza. Hii ni imani potovu. Anasahau kuwa alipewa ubongo wa kuwaza na kuwazua kabla ya kufanya chochote. Dhiki, maradhi na ufukara zimehamia kwa binadamu na kumtia kiwewe’

Binadamu amefyeka misitu kwa kutaka makao, mashamba, mbao, makaa, ujenzi wa nyumba na barabara na mahitaji mengine mengi. Wanyama wamefurushwa na wengi kuangamia kwa sababu ya ukosefu chakula na wengine kushindwa kuhimili mabadiliko katika mazingira. Chemichemi za maji zimekauka nalo jangwa limeanza kutuzuru kwa kasi inayotisha. Kazi ya binadamu imekuwa ya kusukia kamba motoni. Itambidi aanze kujenga kwa matofali ya barafu.

a) Bila kupoteza maana iliyokusudiwa na mwandishi wa taarifa, fupisha aya ya kwanza. (alama 5)
(Maneno 40-50)
b) Kwa kuzingatia aya 4 za mwisho, eleza mambo muhimu yanayoshughulikiwa na mwandishi
(maneno 95-105) (alama 8)

15 marks

3. MATUMIZI YA LUGHA (Alama 40)

Jibu maswali yafuatayo.
3.

Taja vigezo vitatu vya kuainisha konsoonanti za Kiswahili.

3 marks

4.

Onyesha shadda katika maneno yafuatayo

i. Insha
ii. Sanaa

3 marks

5.

Kwa kutoa mifano onyesha matumizi mawili ya vifungo

2 marks

6.

Ainisha viambishi katika neon lifuatalo
Hamkuwalisha

3 marks

7.

Tumia kiunganishi cha uteuzi katika sentensi.

2 marks

8.

Tumia kivumishi-ingineo katika ngeli ya I-I katika sentensi.

2 marks

9.

Andika upya sentensi ifuatayo kwa kutumia kitenzi ndi-
Sisi tulipanga mkutano huo.

2 marks

10.

Tumia kirejeshi cha kati kuunganisha sentensi hizi
Mgeni amefika mapema
Mgeni amekaribishwa

2 marks

11.

Andika udogo na ukubwa wa neon ukuta.

2 marks

12.

Tunga sentensi ukitumia kitenzi –ja kubainisha kauli ya kutendewa.

2 marks

13.

Tumia kiwakilishi kisisitizi cha nomino uteo katika umoja, katika sentensi.

2 marks

14.

Eleza maana ya kishazi.

2 marks

15.

Changanua sentensi ifuatayo kwanjia ya mistari.
Wanafunzi wanashangilia bali wengine hawafurahii.

4 marks

16.

Unda nomino ya dhahania kutoka vitenzi vifuatavyo
i. Dharau
ii. –wa

2 marks

17.

Eleza maana mbili za sentensi ifuatayo.
Amenipigia ngoma

2 marks

18.

Andika hii sentensi kwa wingi. Hakimu alimhukumu seremala aliyeiba samani.

2 marks

19.

Andika kwa usemi wa taarifa.
“ninaumwa na kichwa sana leo.” Mwalimu alisema.

3 marks

20.

Andika neon linguine lenye maana sawa:
Piku

1 marks

4.ISIMU JAMII (Alama 10)

21.

a) Kwa nini kulikuwa na haja ya kusanifisha lugha ya Kiswahili. Toa sababu tano. (alama 5)
b) ….sote tunajua kwamba ni kudura. makiwa!
i. Tambua sajili iliyotumika katika dondoo hili. (alama 1)
ii. Eleza sifa nne za sajili hiyo. (alama 4)

10 marks

Back Top